Azory Gwanda aongoza orodha ya walioathirika na tisho la vyombo vya habari duniani

Azory Gwanda, mwanahabari wa kujitegemea wa Tanzania aliyetoweka kwa zaidi ya miezi 18 anaongoza orodha ya walioathirika na tishio kwa vyombo vya habari kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Umoja wa vyombo huru vya habari wa One Free Press Coalition.
Nick Turner wa Bloomberg News aliripoti Juni 3,2019 kwamba orodha ya dharura ya mwezi inajumuisha pia suala la mwanahabari wa Washington Post, Jamal Khashoggi, aliyeuawa katika ubalozi mdogo wa Saudi Arabia mjini Istanbul, Uturuki mwezi Oktoba mwaka jana. Mauaji hayo hayajafanyiwa uchunguzi huru na Umoja wa Mataifa, kundi hilo limeeleza.
Bloomberg News ni miongoni mwa vyombo vya habari, ikiwemo BuzzFeed na Washington Post vilivyojiunga na Umoja huo wa One Free Press Coalition mwezi uliopita. Mashirika ya habari ya Associated Press, Reuters na gazeti la Financial Times ni sehemu ya umoja huo unaolenga kuinua uelewa kuhusu vitisho dhidi ya uhuru wa habari duniani kote.
Gwanda aliyekuwa akiandikia kampuni ya Mwananchi Communications, wachapishaji wa magazeti ya Mwananchi na The Citizen newspapers kutoka Kibiti Kibiti, Mkoa wa Pwani alitoweka tangu Novemba 2017 na serikali ya Tanzania bado haijaeleza kuhusu wapi alipo.
Wadau wa habari nchini wakiongozwa na umoja wa Haki ya Kupata Taarifa (CoRI) inayoongozwa na Baraza la habari Tanzania (MCT) wameanzisha jitihada za kukusanya saini kwa lengo la kushinikiza serikali kuchukua hatua za kumtafuta Gwanda na kueleza matokeo yake kwa umma.
Hii hapa ni orodha ya dharura muhimu kwa mwezi Juni:
- Azory Gwanda, mwandishi wa kujitegemea wa Tanzania aliytoweka tangu Novemba 2017. Alikuwa akichunguza habari za mauaji katika eneo alilokuwa akifanyakazi.
- Jamal Khashoggi, alieuawa katika Ubalozi mdogo wa Saudi Arabia ulioko Istanbul, Uturuki.
- Aasif Sultan, mwandishi wa Kashmir Narrator aliyekamatwa kwa tuhuma dhidi ya serikali Agosti 2018.
- Claudia Duque, mwandishi wa Colombia anayenyanyaswa kwa miaka kadhaa.
- Miguel Mora na Lucía Pineda wa gazeti la 100% Noticias la nchini Nicaragua ambao wameshikiliwa kwa zaidi miezi mitano kwa tuhuma za kuchochea “ chuki na vurugu”.
- Truong Duy Nhat, mwanamtandao wa Radio Free Asia ambaye ametoweka tangu Januari, Bangkok, Thailand.
- Sevinc Osmanqizi,anayenyanyaswa na kituo cha runinga cha Real TV kinachounga mkono serikali ya Azerbaijani.
- Abderrahmane Weddady na Cheikh Ould Jiddou, wako gerezani tangu Machi nchini Mauritania kwa tuhuma ya kusambaza habari zisizo za kweli.
- Seyoum Tsehaye, aliyekamatwa baada ya serikali ya Eritrea kupiga marufuku vyombo vya habari bianfsi mwaka 2001.
- Mina Karamitrou, mwandishi wa polisi kwa Idara ya Kigiriki ya CNN ambaye alipigwa na bomu lililotegwa kwenye gari.